Brandon Toropov, Mkristo wa Zamani, Marekani (sehemu ya 1 kati ya 2)

Ukadiriaji:
Ukubwa wa herufi:
A- A A+

Maelezo: Jitihada za mtu binafsi za kujifunza mistari halisi zaidi ya Biblia, mistari ya Q, zinamwongoza kwa Uislamu. Sehemu ya kwanza: Tatizo la Ukristo wa kisasa.

  • Na Brandon Toropov
  • Iliyochapishwa mnamo 14 Dec 2021
  • Ilirekebishwa mara ya mwisho mnamo 18 Nov 2021
  • Ilichapishwa: 0
  • Imetazamwa: 1,886
  • Ukadiriaji: bado hakuna
  • Imekadiriwa na: 0
  • Imetumwa kwa barua pepe: 0
  • Ilitoa maoni kuhusu: 0
Mbaya Nzuri zaidi

Wimbi la Waongofu

Kama wewe ni Mkristo, wazo la kwamba Yesu, rehema na baraka za Mungu ziwe juu yake, alikuwa na dini ambayo vyombo vya habari vya leo vinaituhumu kuwa imeleta matatizo mengi ya dunia, inaweza kuonekana kuwa madai yasiyo na msingi. Mimi pia niliyaona hivyo mara ya kwanza nilipokutana nayo, kabla sijasoma Injili zote kwa kina. Hata hivyo unapaswa kujua kwamba Wakristo wengi wa kisasa wamechukua uamuzi wao binafsi uliobadilisha maisha yao kuhusu ujumbe wa Injili na uhusiano wake na Uislamu.

“Kuna uthibitisho wa kuaminika unaoashiria kuongezeka kwa wanaoingia katika Uislamu tangu Septemba 11, si tu katika Uingereza, lakini kote Ulaya na Amerika. Kituo kimoja cha Kiislamu cha Uholanzi kinadai ongezeko la mara kumi, huku Mradi wa Waislamu Mpya, ulio na makao yake Leicester na unaoendeshwa na mama mmoja wa Ireland aliyekuwa Mkatoliki wa zamani, ukiripoti watu wengi wanaojiunga na Waislamu. (London Times, Januari 7, 2002.)

Vyombo Vikuu vya Habari Vinatupuuza

Ni nadra sana kwa Vyombo vya habari vya Magharibi kushiriki na dunia kwa ujumla hadithi za watu hawa wanaoingia katika Uislamu, lakini ninaamini kwamba wengi wa watu hawa -- iwapo wao ni kama mimi -- walijikuta, mwishoni mwa siku, wakiwa na wasiwasi juu ya matokeo ya kumwita Yesu “Bwana” bila kutii maelekezo yake... walijikuta na wasiwasi zaidi kuhusu hilo, kuliko habari yoyote ya vyombo vya habari ya masuala ya kijiografia na kisiasa.

Aina hii ya wasiwasi husababisha watu kubadilisha maisha yao.

Changamoto za Q

Nikijizungumzia mimi binafsi, nilibadilisha maisha yangu mwenyewe kwa sababu sikuweza kupuuza maana ya vifungu halisi vya Injili ambavyo wasomi wakubwa wa leo (wasio Waislamu!) wanaamini kuwa ni vya tarehe ya mbali kabisa kati ya vingine vyote vinavyopatikana.

Maneno haya, ambayo yanaunda maandishi yaliyojengwa upya yanayojulikana kama Q, yanaweza kupatikana yote katika Agano Jipya. Maneno haya ndiyo yaliyo karibu zaidi na maneno halisi ya Yesu, rehema na baraka za Mungu ziwe juu yake, kuliko mengine yoyote yanayoweza kupatikana.

Q Inathibitisha Uislamu

Ikiwa ni mara yako ya kwanza kujua Q, unapaswa kujua kile wasomi bora wa Agano Jipya sasa wanajua, yaani kwamba usomi wa leo unatambua kwamba vifungu fulani vya Injili ni muhimu sio tu katika kufundisha, bali ni muhimu zaidi kihistoria kuliko vifungu vingine. Usomi huu umesababisha majadiliano ya kuvutia kati ya wasomi (na wasomaji wachache wa kawaida).

Naamini aya za Q zinathibitisha taswira ya Uislamu ya Yesu ya kuwa alikuwa Nabii wa kibinadamu mwenye ujumbe wa Kiungu, ambao kimsingi hauna tofauti na ule wa Muhammad, rehema na baraka za Mungu ziwe juu yake.

Nabii Mwanadamu

Sikuendeleza nadharia ya Q. Imekuwa kote kwa miaka sasa. Makasisi wa “Kijadi” wa Kikristo na wanatheolojia kwa ujumla wanaichukia. Wanadai kwamba wanafunzi wa Q kwa namna fulani wanataka kupunguza hadhi ya Yesu, amani iwe juu yake. Kinyume na hiyo, sisi tuna nia ya kujifunza aliyoyasema kihalisi.

Q inawakilisha changamoto kubwa kwa Ukristo wa kisasa, sio tu kwa sababu inaonyesha wazi kwamba taswira ya Uislamu ya Yesu ni sahihi kihistoria. Naamini kwamba ukweli wa kuwa Q kimsingi inathibitisha taswira ya Uislamu ya Yesu kama Nabii mwanadamu haujaonekana vizuri na Wakristo wa leo. Na ni lazima uwe. Kwa sababu mapitio ya makini ya maandiko yanaonyesha kwamba Yesu kwa kweli anawaita watu wake kwa Uislamu.

Yesu alinileta kwa Uislamu!

Nimekuja kwa Uislamu, Alhamdulillah [wa kutukuzwa ni Mwenyezi Mungu] baada ya miongo mitatu ya kutoridhika na Ukristo. Ingawa nimesoma hadithi nyingi za waliokubali uislamu tangu nilipoingia katika Uislamu mwezi Machi mwaka wa 2003, sijaona wengi ambao walitaja Injili kama chanzo chao cha kuingia katika Qurani Tukufu. Hivi ndivyo ilivyokuwa kwangu.

Nilivutiwa na Injili katika umri mdogo -- kumi na moja -- na nikazisoma kwa bidii peke yangu, licha ya kwamba sikuishi katika nyumba ya Kikristo. Baada ya muda mchache nilijifunza kujiwekea mambo ya kidini kivyangu.

Maswali ya Mapema

Ujanani mwangu nilijifunza maandiko ya Kikristo peke yangu. Bado nina bibilia nyekundu ya King James niliyonunua nikiwa mdogo; andiko langu lililoandikwa kwa hati yangu kwenye ukurasa wa mbele inatangaza Juni 26, 1974, kama tarehe niliyomkubali Yesu kama mwokozi wangu binafsi.

Ninaposema nilisoma maandiko kwa kiasi kikubwa, namaanisha kuwa nilivutiwa na Injili za Matayo, Marko, Luka, na Yohana kama sumaku. Kuna maelezo mengi na maandiko yangu katika Biblia yangu ya zamani katika Zaburi, Mhubiri, na Mithali - lakini maelezo mengi na maandiko yapo katika Injili. Lakini nilihisi, hata nikiwa mdogo, kwamba kulikuwa na matatizo ya ndani kwenye maandiko niliyoyapenda sana.

Ni nani aliyebadilisha Injili?

Naweza kukumbuka vizuri nikisoma habari katika sura ya 22 ya Luka ambapo Yesu aliondoka kutoka kwa wanafunzi, akaomba, akarudi na kuwakuta wakiwa wamelala. Ni nani, nilishangaa, angeweza kumwona akisali... na kisha kulihusisha tukio hilo ili hatimaye liingizwe katika Injili ya Luka? Kuna kifungu kingine katika Injili ambapo Yesu anadhaniwa kuweka maneno “wacha anayesoma aelewe” katika moja ya mazungumzo yake, jambo lililoonekana kuwa lisilo la kawaida kwangu. Na bado kulikuwa na kwingine ambapo mwandishi wa Agano Jipya aliwahakikishia Wakristo wa karne ya kwanza kwamba kizazi chao kingeona ujio wa pili wa Masihi - kifungu ambacho nimeona vigumu kuwiana na mafundisho ya kisasa ya Kikristo. Maswali haya na mengine kuhusu Agano Jipya yalitokea nilipokuwa bado mdogo kabisa, hata kabla sijafikisha miaka kumi na mitano. Je, kuna mtu aliyebadilisha Injili? na iwapo yupo, ni nani? Na kwa nini?

Nilijiwekea maswali yangu ili niyashughulikie baadaye, na kuamua kwamba tatizo halisi ni kwamba sikuwa baadhi ya wanachama cha imani chenye nguvu cha Kikristo.

Mkatoliki

Nilipofikisha umri wa miaka kumi na minane, nilielekea Mashariki ili kujiunga na chuo kikuu na kuingia Kanisa Katoliki la Kirumi. Katika chuo kikuu, nilikutana na msichana mzuri na mwenye huruma ambaye alikuwa mkatoliki; na angekuwa mpenzi na msaidizi wangu mkubwa maishani; hakuwa hasa mtu wa dini, lakini alithamini jinsi mambo haya yalivyokuwa muhimu kwangu, na hivyo aliniunga mkono katika imani zangu. Kwa hakika, Kufupisha mwanzo wa uhusiano wetu katika sentensi chache hapa ni udhalimu mkubwa kwa rasilimali zake zisizokuwa na kikomo za nguvu, msaada, na upendo.

Mkutano na Kuhani

Nilimuuliza kuhani wa chuo kikuu - mtu mzuri na mcha Mungu - kuhusu baadhi ya nyenzo za Injili ambazo zilinipa changamoto, lakini akawa na wasiwasi na kubadilisha maudhui. Katika tukio jingine, nakumbuka nikimwambia kwamba nilikuwa nikisoma kwa kina Injili ya Yohana kwa sababu Injili hiyo ilikuwa (kama nilivyofikiri wakati huo) ni maelezo ya binafsi ya matukio hayo.

Kama awali, alibabaika na kubadilisha maudhui na hakutaka kujadili ubora wa Injili moja juu ya nyingine; alisisitiza tu kwamba zote nne zilikuwa muhimu na kwamba nizisome zote. Haya yalikuwa mazungumzo muhimu, na bainishi, kama nilivyokuja kujua baadaye.

Ukristo au Upaulo?

Hii sio hadithi ya maisha yangu, bali ni maelezo ya wongofu wangu, kwa hivyo nitaruka matukio mengi muhimu. Kuhani huyo mzuri hatimaye alifunganisha ndoa yetu mimi na mpenzi wangu, na tukahamia viunga vya Massachusetts. Kila mmoja wetu alijiendeleza mbele kitaaluma na tukakua. Tulikuwa na watoto watatu wazuri. Na niliendelea kusoma Biblia kila mara. Nilivutiwa na maneno kuhusu taa na jicho, Mwana Mpotevu, Heri, umuhimu wa sala, na mengine mengi - lakini nilikuwa na matatizo makubwa zaidi ya kimantiki na “usanifu” unaozunguka Agano Jipya, hasa kwa Mtume Paulo. Ukweli kwamba Paulo hakuonekana kujenga hoja ya kitheolojia karibu na chochote ambacho Yesu alisema kihakika ulikuwa tatizo kubwa sana kwangu.

Katikati ya miaka ya 1990, mimi na mke wangu sote tulivunjika moyo sana na Kanisa Katoliki, na sababu kubwa ni kutokana na kuhani mmoja mbaya ambaye hakuyapea kipaumbele mahitaji ya kiroho ya jamii yake. Baadaye tulikuja kujua kwamba alikuwa akimsitiri mnyanyasaji wa mtoto!

Mprotestanti

Niliona ni muhimu kujitumbukiza katika jamii ya imani. Nilijiunga, na nikawa mwenye bidii, katika dhehebu la Kiprotestanti, amablo ni Kanisa la Kutaniko.

Kwa hivyo niliongoza madarasa ya Shule ya Jumapili kwa watoto, na kwa kifupi nilifundisha darasa la Injili kuhusu Mifano kwa watu wazima. Katika madarasa ya Shule ya Jumapili kwa watoto nilifuata vizuri mtaala niliopewa; lakini katika darasa la watu wazima, nilijaribu kuwashawishi washiriki kujiuliza maswali kuhusu Mifano fulani moja kwa moja, bila kuchuja kila kitu kupitia Mtume Paulo. Tulikuwa na majadiliano ya kuvutia, lakini nilihisi upinzani fulani, na sikujaribu kufundisha darasa la watu wazima tena. Mke wangu hatimaye alijiunga na kanisa langu. (Yeye ni mwanachama huko leo.)

Kwa hatua hii, nilikuwa nimeathiriwa sana na uwiano ulio dhahiri kati ya mila ya kifumbo ya Kikristo na ile ya Wasufi na Wabudha wa Zen. Hadi nilikuwa nimeandika kuhusu mambo hayo. Lakini hakukuonekana kuwa na mtu yeyote katika kanisa langu ambaye alishiriki bidii yangu kwa masuala haya.

Mbaya Nzuri zaidi

Brandon Toropov, Mkristo wa zamani, Marekani (sehemu ya 2 kati ya 2)

Ukadiriaji:
Ukubwa wa herufi:
A- A A+

Maelezo: Jitihada za mtu binafsi za kujifunza mistari halisi zaidi ya Biblia, mistari ya Q, zinamwongoza kwa Uislamu. Sehemu ya pili: Ulinganisho na Qur'ani.

  • Na Brandon Toropov
  • Iliyochapishwa mnamo 14 Dec 2021
  • Ilirekebishwa mara ya mwisho mnamo 18 Nov 2021
  • Ilichapishwa: 0
  • Imetazamwa: 2,030
  • Ukadiriaji: bado hakuna
  • Imekadiriwa na: 0
  • Imetumwa kwa barua pepe: 0
  • Ilitoa maoni kuhusu: 0
Mbaya Nzuri zaidi

Kuzingatia Maneno ya Injili kwa Makini

Hususan, nilikuwa nikifuatilia kwa makini utafiti uliofanywa ambao ulionyesha kuwa matabaka ya zamani zaidi ya Injili yalionyesha chanzo cha mdomo cha mapema sana kinachojulikana kama Q, na kwamba kila kundi la maneno ya Yesu, rehema na baraka za Mungu ziwe juu yake, linahitajika kutathminiwa kwa sifa zake lenyewe, na sio kama sehemu ya nyenzo simulizi zilizolizunguka.

Hii ni kwa sababu nyenzo hizo simulizi ziliongezwa miaka mingi baadaye.

Simulizi ya Shahidi?

Kwa kweli, nilivyotafiti somo hili kwa zaidi, ndivyo nilivyojikuta nikifikiria mazungumzo hayo kuhusu Injili ya Yohana kati yangu mimi na kuhani wangu. Nilitambua kwamba kile ambacho hakutaka au hakuweza kuniambia ni kwamba mwandishi/waandishi wa Injili ya Yohana walidanganya. Ilikuwa wazi kuwa hayo siyo masimulizi ya shahidi, ingawa wailidai hivyo.

Nilikuwa katika hali ya ajabu. Kwa hakika nilifurahia ushirika wa Wakristo katika kanisa langu, ambao wote walikuwa watu wenye nia nzuri na wenye kusali. Kuwa mwanachama wa jumuiya ya kidini ilikuwa muhimu kwangu. Hata hivyo nilikuwa na shaka kubwa kimantiki kuhusu historia inayodaiwa ya simulizi za Injili. Zaidi ya hayo, nilikuwa nikizidi kupata ujumbe tofauti kutoka kwa maneno ya Yesu katika Injili kuliko ule ambao Wakristo wenzangu walikuwa wakiupata.

Kukabiliana na Mafundisho ya Utatu

Nilivyozidi kutazama maneno haya, ndivyo nilivyopata ugumu kupatanisha dhana ya Utatu na ile ambayo ilionekana kwangu kuwa ya kweli katika Injili. Nilijikuta nikikabiliana uso kwa uso na maswali magumu sana.

Ni wapi katika Injili Yesu alitumia neno “Utatu”?

Ikiwa Yesu alikuwa Mungu, kama vile mafundisho ya Utatu yanadai, kwa nini alimwabudu Mungu?

NA - kama Yesu alikuwa Mungu, kwa nini aseme kitu kama kifuatacho?

“Mbona unaniita mwema? Hakuna aliye mwema isipokuwa Mungu peke yake.” (Marko 10:18)

Je, kuna uwezekano, kwa namna fulani, alisahau kwamba yeye mwenyewe alikuwa Mungu wakati aliposema haya?

(Maelezo ya kando -- Nilikuwa na mazungumzo na mwanamke fulani aliyenihakikishia kwamba kifungu hiki hakikuwa katika Injili, na alikataa kuamini kwamba kilikuwa pale mpaka nilipompa sura na namba ya mstari na akaiangalia mwenyewe!)

Qur'ani Takatifu

Mnamo mwezi wa Novemba mwaka wa 2002, nilianza kusoma tafsiri ya Qurani.

Sijawahi kusoma tafsiri ya Kiingereza ya maandishi yote ya Qurani kabla ya hapo. Nilisoma tu muhtasari wa Qurani ulioandikwa na wasio Waislamu. (Na ulikuwa muhtasari wa kupotosha sana.)

Maneno hayaelezei kwa kutosha athari ya ajabu ambayo kitabu hiki kilikuwa nayo kwangu mimi. Inatosha kusema kwamba mvuto ule ambao ulinivuta kwa Injili katika umri wa miaka kumi na moja ulikuwepo kwa namna mpya na yenye maana kubwa sana. Kitabu hiki kilikuwa kinaniambia, kama vile nilivyoweza kujua kuwa Yesu alikuwa akiniambia, kuhusu mambo yaliyo muhimu kabisa.

Mwongozo Imara

Qurani ilikuwa ikitoa mwongozo imara na majibu halisi kwa maswali niliyokuwa nikiyauliza kwa miaka mingi kuhusu Injili.

“Haiwezi kuwa mtu aliye pewa na Mwenyezi Mungu Kitabu na hikima na Unabii kisha awaambie watu: Kuweni wa kuniabudu mimi badala ya Mwenyezi Mungu. Bali atawaambia: Kuweni wenye kumuabudu Mola Mlezi wa viumbe vyote, kwa kuwa nyinyi mnafundisha Kitabu na kwa kuwa mnakisoma. Wala hatakuamrisheni kuwafanya Malaika na Manabii kuwa ni miungu. Je, atakuamrisheni ukafiri baada ya kuwa nyinyi Waislamu?” (Kurani 3:79-80)

Qurani ilinivuta kwa ujumbe wake kwa sababu ilithibitisha vizuri maneno ya Yesu ambayo nilihisi moyoni mwangu yalikuwa ya kweli. Kuna kitu kilibadilishwa katika Injili, na kitu hicho, nilijua katika moyo wangu, kilikuwa kimesalia kama kilivyokuwa awali katika maandishi ya Qurani.

Usambamba wa Kushangaza

Chini utapata mifano michache tu ya ulinganifu uliofanya moyo wangu uelekee kwa ibada ya Mungu. Kila mstari wa Injili unakuja na maandishi yaliyojengwa upya yanayojulikana kama matini ya-- Q ambayo wasomi wa leo wanaamini yanawakilisha tabaka la mwanzo kabisa la mafundisho ya Masihi. Angalia jinsi nyenzo hii ilivyo karibu na ujumbe wa Qurani.

Q Inakubaliana na Qur'ani juu ya Tawheed (Umoja wa Mungu)

Katika Q, Yesu anathibitisha, kwa maneno yasiyo na utata, umoja wa mungu.

“Nenda nyuma yangu, Ewe Shetani; maana imeandikwa, msujudie Bwana Mungu wako, na umwabudu yeye peke yake.” (Luka 4:8)

Linganisha:

“Je! Sikuagana nanyi, enyi wanaadamu, kuwa msimuabudu Shet'ani? Hakika yeye ni adui dhaahiri kwenu. Na ya kwamba mniabudu Mimi? Hii ndiyo Njia Iliyo Nyooka"(Kurani 36:60-61)

Q Inakubaliana na Qur'ani Kuhusu Aqaba (Njia ya Kupanda Mlima)

Q inabainisha njia iliyo nyooka ambayo mara nyingi ni ngumu, njia ambayo makafiri watachagua kutofuata.

““Ingieni kwa kupitia mlango mwembamba; kwa maana mlango mpana na njia rahisi huelekea kwenye maangamizo, na watu wanaopitia huko ni wengi. Lakini mlango mwembamba na njia ngumu huelekea kwenye uzima, na ni wachache tu wanaoiona.” (Mathayo 7:13 -14)

Linganisha:

“Walio kufuru wamepambiwa maisha ya duniani; na wanawafanyia maskhara walio amini. Na wenye kuchamngu watakuwa juu yao Siku ya Kiyama...” (Kurani 2:212)

“Na nini kitakujuvya ni nini njia ya vikwazo vya milimani? Kumkomboa mtumwa. Au kumlisha siku ya njaa,Yatima aliye jamaa, Au masikini aliye vumbini. Tena awe miongoni mwa walio amini na wakausiana kusubiri na wakausiana kuhurumiana.” (Kurani 90:12-17)

Q Inakubaliana na Qur'ani Kuhusu Taqwa (Kumcha Mwenyezi Mungu)

Q anatuonya tuogope tu hukumu ya Mungu.

“Nawambieni rafiki zangu, msiwaogope wale wauao mwili, na halafu basi. Lakini nitawaambia nani wa kumwogopa: mwogopeni yule ambaye baada ya kumwua mtu ana mamlaka ya kumtupa motoni. Naam: huyo, mwogopeni!” (Luka 12:4 -5)

Linganisha:

“Na ni vyake Yeye viliomo katika mbingu na ardhi. Na Dini ni yake Yeye daima. Je! Mtamcha mwengine asiye kuwa Mwenyezi Mungu?” (Kurani 16:52)

Q Inakubaliana na Qur'ani Kuhusu Mitego ya Dunya (Maisha ya Dunia)

Katika Q, Yesu anawaonya wanadamu waziwazi kwamba faida za kidunia na raha hazipaswi kuwa lengo la maisha yetu:

“Lakini ole wenu ninyi matajiri, kwa sababu mmekwisha pata furaha yenu! Ole wenu ninyi mlioshiba, maana mtaona njaa! 25 Ole wenu ninyi mnaocheka sasa, maana mtalia na kuomboleza.” (Luka 6:24)

Linganisha:

“Kumekushughulisheni kutafuta wingi, Mpaka mje makaburini! . Sivyo hivyo! Mtakuja jua! Tena sivyo hivyo! Mtakuja jua! Sivyo hivyo! Lau mngeli jua kwa ujuzi wa yakini, Basi bila ya shaka mtaiona Jahannamu! Tena, bila ya shaka, mtaiona kwa jicho la yakini. Tena bila ya shaka mtaulizwa siku hiyo juu ya neema.” (Kurani 102:1-8)

Q Inawaonya Watu Wasidhani Wana Uhakika Wataingia Mbinguni!

Fikiria pia maneno yafuatayo kutoka kwa Masihi, ambayo yanapaswa (!) yaufanye kila moyo uwe mnyenyekevu, yaondoe kila aina ya kiburi katika masuala ya kiroho, na yanyamazishe kila shambulio lolote juu ya muumini mwingine:

“Ninawahakikishia kwamba wengi watatoka mashariki na magharibi nao wataketi mezani pamoja na Ibrahimu, Isaka na Yakobo katika Ufalme wa mbinguni. Lakini wanaoamini ufalme wa mbinguni ni wao, watatupwa nje gizani, huko watu watalia na kusaga meno.” (Matayo 8:11 -12)

Ni wazi kwamba, haya ni mafundisho muhimu kwa watu wote wenye nia nzuri wazingatie... na kuyakumbuka daima.

Q Haisemi Chochote Kuhusu Kusulubiwa au Dhabihu!

Umeona jinsi aya za awali kabisa katika historia --aya za Q --yanaenda sambamba na mafundisho makuu ya Qur'ani. Pia ni muhimu kutaja ukweli kwamba Q haifundishi chochote kuhusu kusulubiwa kwa Yesu, au asili ya kidhabihu ya utume wa Yesu... na kuondolewa kwa hayo ni jambo la kusisimua kweli!

Tunabaki basi na Injili ya awali kabisa -- Injili ambayo wasomi (wasio Waislamu) wanaamini ni karibu sana na Yesu kihistoria -- Injili ambayo ina sifa zifuatazo:

Ukubaliano na ujumbe wa Qur'ani usio na kigeugeu kuhusu umoja wa Mungu.

Ukubaliano na ujumbe wa Qurani kuhusu maisha ya baadaye ya wokovu au maangamizi kwenye moto... kulingana na matendo yetu duniani.

Ukubaliano na onyo la Qur'ani dhidi ya kupotoshwa na duniya -- vishawishi na raha za maisha ya kidunia.

Na...

UKOSEFU kamili wa kumbukumbu yoyote kuhusu kifo cha Yesu msalabani, ufufuo, au dhabihu kwa ajili ya wanadamu!

Hii ndiyo Injili ambayo wasomi wakubwa wa leo wasio Waislamu wametubainishia... na Injili hii inatuelekeza, iwapo tu tutasikiliza, kwa mwelekeo sawa na Qurani!

Ndugu na dada zangu wapendwa wa Kikristo, nawasihi kuomba kwa sala, kutafuta mwongozo wa Mungu juu ya swali hili: Je, hii inaweza kuwa tukio la kibahati tu?

Tangaza Neno!

Niliingia Uislamu tarehe 20 Machi, 2003. Ilikuwa dhahiri kwangu kwamba nilipaswa kushiriki ujumbe huu na Wakristo wengi iwezekanavyo wenye kufikiria.

Mbaya Nzuri zaidi

Sehemu za Makala hiki

Ongeza maoni

  • (Haitaonyeshwa kwa umma)

  • Maoni yako yatakaguliwa na yanapaswa kuchapishwa ndani ya saa 24.

    Sehemu zilizo na alama ya nyota (*) zinahitajika.

Iliyotazamwa Zaidi

Kila siku
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
jumla
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)

Chaguo la Mhariri

(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)

Orodha Yaliyomo

Tangu ulivyo tembelea mara ya mwisho
Orodha hii ipo tupu kwa sasa.
Zote kwa tarehe
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)

Maarufu sana

Iliyokadiriwa juu zaidi
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
Iliyotumwa  kwa barua pepe zaidi
Iliyochapishwa zaidi
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
(Soma zaidi...)
Iliyotolewa maoni zaidi

Unazozipenda

Orodha ya unazozipenda ipo tupu. Unaweza kuongeza makala kwenye orodha hii kwa kutumia zana za makala.

Historia yako

Orodha yako ya historia ipo tupu.